Tangazo

April 27, 2015

NAIBU IGP AHIMIZA MAFUNZO KUUKABILI UHALIFU MPYA

Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi, Abdulrahmani Kaniki akisalimiana na baadhi ya Wakufunzi wa chuo cha Polisi Moshi (CCP) wakati alipokuwa katika ziara ya kikazi kukagua mafunzo yanayoendelea chuoni hapo.Kushoto ni Mkuu wa Chuo hicho, Kamishna msaidizi mwandamizi wa Polisi (SACP) Matanga Mbushi.(Picha na Frank Geofray wa Jeshi la Polisi)


Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi, Abdulrahmani Kaniki (kushoto) akiwasili katika chuo cha Polisi Moshi (CCP) wakati alipokuwa katika ziara ya kikazi kukagua mafunzo yanayoendelea chuoni hapo.Katikati ni Mkuu wa Chuo hicho, Kamishna msaidizi mwandamizi wa Polisi (SACP) Matanga Mbushi na Mkuu wa Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Naibu Kamishna Omar Rashid (Picha na Frank Geofray wa Jeshi la Polisi)
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx
Na Frank Geofray-Jeshi la Polisi, Moshi.

Wakufunzi wa Chuo cha Polisi Moshi (CCP) wametakiwa kuendelea kutoa mafunzo kwa weledi ili kuweza kupata askari bora ambao watashirikiana na jamii katika kupambana na uhalifu hasa katika kipindi hiki ambapo kumeibuka uhalifu mpya kwa njia ya mitandao na unaovuka mipaka.

Wito huo umetolewa jana mjini moshi na Naibu Inspekta Jenerali wa  Polisi, Abdulrahman Kaniki wakati alipokuwa katika ziara ya kikazi chuoni hapo ambapo alizungumza na wakufunzi hao na kuweka mikakati mbalilmbali ya kuboresha mafunzo katika chuo hicho.

Naibu IGP Kaniki alisema, askari wakipata mafunzo bora wataongeza mbinu zitakazowezesha kukabiliana na  uhalifu huo na hivyo kuendelea kuimarisha usalama wa raia na mali zao kwa kushirikiana na jamii ambayo imekuwa msaada mkubwa wa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu.

“Ili kuhakikisha kwamba raia wa Tanzania na mali zao wanalindwa ipasavyo, Jeshi la Polisi hatuna budi kuendelea kubuni mbinu mpya za kukabiliana na uhalifu wa kila aina unaobadilika mara kwa mara na hilo linawezekana kwa kuendelea kuwapatia askari wetu mafunzo yenye viwango vya kupambana na uhalifu unaokua kwa kasi”alisema Kaniki.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Polisi moshi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Matanga Mbushi alisema wanaendelea na juhudi za kuhakikisha kuwa mafunzo wanayotoa yanalenga katika mitaala ambayo wamekuwa wakiiboresha mara kwa mara ili kuendana na wakati kulingana na mazingira ya uhalifu unaotokea katika jamii.

Alisema, mbinu za uhalifu zimekuwa zikibadilika kila siku hivyo, na wao kama chuo wamejikita kuhakikisha kuwa askari wanaopita katika chuo hicho wanazipata mbinu mpya na hivyo kuwa zaidi ya wahalifu ili waweze kupambana nao.


 

No comments: