Tangazo

March 4, 2015

KATIBU MKUU KIONGOZI AFURAHISHWA NA UWEPO WA SACCOS MAKAZINI

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue (kushoto) akimsikiliza Mshauri Mkuu na Mlezi wa Ikulu SACCOS Bw Joseph Sanga (wa pili kulia) akimuelezea mikakati ya ushirika huo wakati wa hafla fupi ya kumkabidhi kitabu chake cha uanachama wa ushirika huo Ikulu Dar es salaam. Wa pili kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa Ikulu SACCOS, Bw. Deodatus Gaudio, akifuatiwa na Katibu wake Bw. Benedicto Damiano na kulia ni Mtunza Hazina Bi. Judith Medson. HABARI NA PICHA/IKULU
Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue akipokea kitabu chake cha uanachama toka kwa Makamu Mwenyekiti wa Ikulu SACCOS, Bw. Deodatus Gaudio (wa tatu toka kulia). Wengine ni Katibu wa wa ushirika huo  Bw. Benedicto Damiano (wa pili kulia),  Mtunza Hazina Bi. Judith Medson ( wapili kushoto)  na Mshauri Mkuu na Mlezi wa Ikulu SACCOS Bw Joseph Sanga kulia,wakati wa hafla fupi ya kumkabidhi kitabu chake cha uanachama wa ushirika huo Ikulu Dar es salaam.

========================
Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amefurahishwa na  uwepo wa vyama vya Ushirika vya Akiba na mikopo (SACCOS) katika taasisi na idara za serikali, akisema kuwa hilo ni jambo la maana kwa kuwa  inatoa fursa kwa watumishi kuwa na kipato cha ziada kitachosaidia kuwaletea ahueni  kwani mishahara pekee  haikidhi matakwa yao yote.

Amesema SACCOS ni ​kama ​benki ya mtu mnyonge, na kusisitiza kwamba mifuko ya aina hiyo inaposimamiwa vizuri faida yake kwa wanachama ni kubwa sana kwani humpa mtumishi ahueni na kumfanya afanye kazi kwa moyo na  bila wasiwasi ama usongo wa mawazo. 

Balozi Sefue ameyasema hayo Jumanne Machi 3, 2015 jioni alipokuwa akiongea na uongozi wa Ikulu SACCOS,​uli​omtembelea ofisini kwake Ikulu Dar es salaam kumkabidhi rasmi kitabu chake cha uanachama kufuatia kujiunga kwake na ushirika huo.

 “Mishahara yetu ndani ya utumishi wa umma haitoshi kukidhi mahitaji yetu yote, kwa hiyo mipango yote hii ya SACCOS, Mfuko wa Rambirambi na Mfuko wa Ushirika ​iliyopo hapa Ikulu inafanya maisha ya mtumishi yawe na ahueni sana na kumfanya afanye kazi kwa moyo. 

“Hayo ni mambo ambayo nayaamini sana na nayaunga mkono;  na naamini hata Mhe Rais mwenyewe anayaunga mkono na ndio maana amekuwa mwepesi kujiunga na ushirika ”, amesema Balozi Sefue baada ya kukabidhiwa kitabu namba 2 na Makamu Mwenyekiti wa Ikulu SACCOS, Bw. Deodatus Gaudio. Kitabu namba moja amekabidhiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete.

Awali, mshauri Mkuu na Mlezi wa Ushirika huo wa Ikulu, Bw. Joseph Sanga, alimfahamisha Katibu Mkuu Kiongozi kwamba  mifuko ya SACCOS, Ushirika wa Nyumba na  Rambirambi ya  watumishi wa Ikulu iko imara na inaendelea kunufaisha wanachama wake kwa ufanisi.

Bw. Sanga amesema malengo makuu ya mifuko hiyo ni kuleta ustawi kwa watumishi na kwamba wote wanaelewa kuwa mikopo ya SACCOS yao sio kwa ajili ya kununulia chakula ama mavazi bali ni ya kuwekeza kwenye miradi itayowaongezea kipato.

“TUnataka kwenda mbali zaidi kwa kushirikiana na mfuko wetu ya Ushirika wa Nyumba ambo tayari umepeleka maombi ya ardhi kwa wanachama wake ambapo viwanja vikipatikana tuna mategemeo ya kuwapa mikopo kuvununua. Mpango huu una faida kwani ni wa amana kubwa na riba ndogo”, alisema Bw. Sanga alipokuwa anafafanua kuhusu mipango ya Ikulu SACCOS.

No comments: